Friday, March 9, 2012

Man U apata Kichapo nyumbani


Mashabiki wa Manchester United walibaki jana vinywa wazi pale timu yao ilipochapwa mabao matatu kwa mbili na Athletico Bilbao katika uwanja wao wa Old Trafford.

Aibu ya kuchapwa nyumbani na Athletico Bilbao

Timu hiyo ya Uhispania iliizidi maarifa mashetani wekundu katika mchuano wa hatua ya timu 16 bora ya mechi za kombe la ligi ya Euro.

Man U ndio waliokuwa wakwanza kufunga bao katika dakika ya 22 kupitia mwamba wake Wayne Rooney. Lakini baada ya hapo Athletico ilianza kuihangaisha ngome ya Manchester United . Na kukiwa kumesalia dakika chache tu kwa timu hizo kwenda mapumziko Fernando Llorente aliisawazishia Athletico Bilbao. Baadae Oscar de Marcos na Iker Muniain wakafanya magoli kuwa 1-3.

Lakini kabla ya kipyenga cha mwisho Rooney aliipatia Man U bao lake la pili kupitia mkwaju wa penalti.

Baada ya mechi hiyo Meneja wa Manchester United akiri kuwa timu yake ilizidiwa maarifa na Athletico Bilbao ya Uhispania.

" Walikuwa wazuri kutushinda . Kwetu itakuwa ni kazi ya kupanda mlima", Ferguson alisema.

Lakini mkufunzi huyo wa Man U bado ni mwingi wa matumaini kwamba wanauwezo wa kifunga Athletico Bilbao watakapowatembelea kwao baada ya wiki mbili.